Sunday, January 15, 2012

Chadema yagubikwa na simanzi:yapoteza mbunge

                                        Mbunge Regia Mtema; enzi za uhai wake 


Mbunge wa Viti Maalumu kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Regia Estelatus  Mtema (32), amefariki dunia baada ya gari alilokuwa akiendesha, kupinduka eneo la Mlandizi, Kibaha mkoani Pwani jana.

Ajali hiyo ilitokea saa 5:30 asubuhi karibu na Sekondari ya Ruvu, wakati mbunge huyo na watu wengine saba, wakisafiri kwa gari aina ya Toyota Landcruiser wakitoka Dar es Salaam kwenda Morogoro.Akielezea mazingira ya ajali hiyo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Ernest Mangu, alisema mbunge huyo alifariki baada ya gari hilo alilokuwa akiendesha mwenyewe, kuacha njia na kupinduka.

Alisema ajali hiyo ilitokea baada ya Mtema kujaribu kulipita gari lililokuwa mbele yake na ghafla aliona gari lingine likija kasi mbele yake,  katika kujaribu kulikwepa, ndipo gari hilo lilipinduka.

"Wakati akiwa hajalipita gari hilo aliliona gari lingine likija mbele kwa kasi , katika kulikwepa wasigongane uso kwa uso, alitoa gari lake barabarani na kusababisha kupinduka,’’ alisema Mangu.

Alisema watu wengine saba  waliokuwa kwenye gari hilo walijeruhiwa, wawili kati yao  hali zao zilikuwa mbaya,  walipelekwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) Dar es Salaam kwa matibabu zaidi, huku wengine watano, wakiwahishwa Hospitali Teule ya Tumbi Kibaha.

                                    Gari iliyopelekea kifo cha mbunge ikiwa 
                                   imepakiwa kituo cha polisi Mlandizi mkoani pwani.

Aliwataja majeruhi waliolazwa Tumbi kuwa ni Lawrence Mtokambali (58), Benadetha Mtema (50), Peter Madesa (50) na Rogers Abdallah(18).

Chadema yatoa tamko
Chadema kilisema kuwa Mtema alikuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama hicho na Waziri Kivuli wa Kazi na  alikuwa mchapa kazi hodari katika majukumu mbalimbali yakiwepo ya kijamii na kisiasa.

Taarifa hiyo iliyotolewa na Chadema jana na kusainiwa na Katibu Mwenezi wa chama hicho, John Mnyika ilieleza kuwa viongozi wakuu wa chama hicho wakiongozwa na Mwenyekiti wao Freeman Mbowe, Katibu Mkuu, Dk Willibroad Slaa, wajumbe wa Kamati Kuu, Wakurugenzi wa chama hicho makao makuu na wabunge, wameshtushwa na kifo hicho na kuungana na familia ya marehemu katika kipindi hiki kigumu cha majonzi.

Chadema kimesema taarifa zaidi kuhusu taratibu za maziko, itatolewa mara baada ya kukamilisha majadiliano kati familia ya marehemu, chama na Ofisi ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kufuatia kifo hicho, mkutano wa Chadema uliokuwa umepangwa kufanyika jana Mjini Kibaha umehirishwa hadi itakapotangazwa wakati mwingine.

Elimu yake
Mtema alizaliwa Aprili 21, 1980. Alisoma elimu ya msingi kati ya mwaka 1989 na 1995. Alijiunga na Shule ya Sekondari Forodhani, Dar es Salaam mwaka 1996 hadi  1999 na kuhitimu kidato cha nne.
Aliendelea kidato cha tano 2002 na sita kati ya mwaka 2000 na 2002 katika Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Machame, mkoani Kilimanjaro.

Mwaka 2003 hadi 2006 alisoma Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA) na kupata Shahada ya Maarifa ya nyumbani na Lishe. Baada ya kuhitimu shahada yake, marehemu Mtema alifanya kazi katika taasisi mbalimbali kabla ya kujiunga na Chadema na kuteuliwa kuwa Ofisa Mwandamizi katika Kurugenzi ya Vijana ya chama hicho.

Baadaye aliteuliwa kuwa Ofisa Mwandamizi katika Kurugenzi ya Mafunzo ya chama hicho, nafasi ambayo aliishikilia hadi mwaka 2010 alipoteuliwa kuwa Mbunge wa Viti Maalum.

JK amtumia rambirambi Mbowe
Wakati huo huo, Rais Jakaya Kikwete amemtumia salamu za rambirambi Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe kufuatia kifo cha mbunge huyo.

Katika salamu hizo, Rais ameelezea kusikitishwa kwake na taarifa za kifo cha mbunge huyo na kueleza kwamba, marehemu Mtema  amepoteza maisha akiwa kijana na kwamba pigo hilo si kwa Chadema pekee bali kwa taifa zima.

“Nimepokea kwa masikitiko na huzuni nyingi habari za kifo cha Mheshimiwa Mtema katika ajali ya gari. Siyo kwamba ajali hii imechukua maisha ya kijana bali imelinyang’anya taifa mbunge hodari, na kwa hakika, kifo chake siyo tu ni pigo kwa chama chako bali ni pigo kwa sote na kwa taifa letu kwa jumla.

"Nakutumia wewe binafsi, chama chako na wanachama wake salamu za dhati ya moyo wangu kuomboleza kifo na msiba huu mkubwa," alisema Rais Kikwete kupitia taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu.

Aliongeza: “Napenda ujue kuwa niko nanyi katika msiba huu. Napenda vilevile uniwasilishie salamu zangu za rambirambi za dhati kabisa kwa wana-familia, ndugu na jamaa wa marehemu Mheshimiwa Mtema.

Taarifa hiyo imemwomba Mbowe kufikisha salamu za Rais Kikwete kwa familia ya mbunge huyo na kuijulisha kuwa amepokea habari hizo kwa huzuni kubwa. "Wajulishe kuwa nawaombea kwa Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, awajalie uvumilivu na subira katika kipindi hiki kigumu kwa sababu yote ni mapenzi yake.

Wananchi wamlilia
Katika kuonyesha kuguswa na kifo hicho mamia ya watu wanaotumia mtandao wa kijamii maarufu kwa jina la ‘Facebook’  walielezea kusikitishwa na kifo hicho huku wakitoa maoni mbalimbali.

Miongoni mwa maelezo yao ni juu ya maneno aliyowahi kuyazungumza mbunge huyo kijana, ukiwamo ujumbe alioandika katika mtandao huo akiwataka wananchi wamweleze kero zao ili azifikishe katika mkutano ujao wa Bunge.

Ujumbe huo aliouandika Januari 10 mwaka huu na kuungwa mkono na watu 159 ulisomeka hivi;

“Wapenzi, habari zenu kama una kero yoyote unayoona inafaa ikasemewe bungeni au nje ya Bunge na Wabunge na Viongozi wa Chadema basi tupia hapa kero yako. Angalizo; isiwe kero binafsi..., karibuni sana pamoja tunaweza”.

Mtema anakuwa mbunge wa pili wa chama hicho kufariki dunia kwa ajali ya gari, Julai 27, 2008 Mbunge mwingine wa chama hicho Jimbo la  Tarime, Chacha Wangwe alikufa katika ajali ya gari eneo la Pandambili mkoani Dodoma.
                                                                                                                     posted by Frank Kimaro
                                 

Thursday, January 12, 2012

Salam kutoka Finland

Waziri wa Habari na Mahusiano ya Umma, TUSO IUCO, Elisha Magolanga akiwa nchini Finland kuhudhuria mafunzo (Exchange programme) katika chuo cha Turku University Applied of Sciences
Katikati ya jiji la Turku, mji

Katika sherehe ya kuwakaribisha wanafunzi wote waliohudhuria exchange programme katika Hotel ya Holiday Inn mjini Turku

Saturday, December 31, 2011

Mwaka uliokua na upinzani mkubwa katika medani ya siasa kati ya CHADEMA na C.C.M

By Frank Kimaro













MWAKA 2011 unamalizika leo na kuacha kumbukumbu ambazo ni vigumu kusahaulika katika medani za siasa nchini, huku baadhi ya vigogo wa kisiasa wakiweka historia kutokana na kukumbwa na matukio ya aina yake.
Katika miezi 12 iliyopita, Taifa limepita katika misukosuko mingi ya kisiasa iliyoanzia Januari 5, pale maadamano ya Chadema yaliyofanyika mjini Arusha yaliposababisha vifo vya watu wanne.

Hilo ni miongoni mwa matukio mengi ya kisiasa ambayo yalikuwa na sura ya mvutano baina ya vyama vya CCM na Chadema, ambavyo hivi sasa vinatoa mwelekeo wa siasa za nchi.

Risasi za moto na mabomu ya machozi vilitumika katika jitihada za polisi kuzima maandamano hayo, wakitekeleza amri ya Mkuu wa Jeshi hilo, Inspekta Jenerali Saidi Mwema ambaye awali alipiga marufuku maandamano hayo kwa madai ya kuwepo uwezekano wa kutokea vurugu.

Kufuatia vurugu hizo, Januari 6 Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk Willibrod Slaa, wabunge wawili wa chama hicho na wafuasi wengine 21, walifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha kujibu mashitaka kuhusu maandamano hayo, kesi ambayo bado inaendelea hadi sasa.

Kiini cha mtafaruku huo ni mvutano kuhusu nafasi ya Meya wa Jiji la Arusha, ambayo Chadema walikuwa wakilalamikia kwamba uchaguzi ulichakachuliwa hivyo kukipa CCM ushindi hivyo kufanya maandamano ya kupinga uchaguzi huo.

Hadi leo suala hilo limebaki kuwa kitendawili kisichokuwa na majibu kwani kumekuwapo kwa migogoro ya chinichini kuhusu suala zima la meya kiasi cha kuathiri shughuli za maendeleo katika mji huo wa kitalii na kibiashara uliopo Kaskazini Mashariki mwa Tanzania.

CCM na Chadema viliendeleza siasa za kupimana ubavu katika uchaguzi mdogo wa Igunga ulitokana na kujiuzulu kwa aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo kupitia CCM, Rostam Aziz, ikiwa ni hatua ya kutekeleza falsafa ya ‘kujivua gamba’ iliyoasisiwa na chama chake ikiwataka watuhumiwa wote wa ufisadi ndani ya chama hicho kuachia ngazi.

Uchaguzi mdogo wa Igunga ulikuwa uwanja mwingine wa mapambano baina ya Chadema na CCM, kwani kuliendeshwa siasa chafu ambazo zilizosababisha baadhi ya watu kujeruhiwa na kufanyiwa vietendo vya kinyama.

Hata hivyo CCM walifanikiwa kutetea jimbo hilo kupitia kwa mgombea wake, Dk Dalaly Kafumu aliyemshinda kwa kura zaidi ya 3,000 mpinzani wake mkuu katika uchaguzi huo, Joseph Kashindye wa Chadema.

Ndani ya Chadema
Katibu Mkuu wa Chadema Dk Willbrod Slaa ambaye alikuwa mgombea urais kupitia chama hicho mwaka jana, amekuwa kimya kwa muda mrefu na ni mara chache kuonekana hadharani akizungumza, isipokuwa katika matukio ya chama chake.

Hali hiyo inatafsiriwa kwamba huenda bado akawa na mpango wa kugombea nafasi hiyo mwaka 2015 akimsubiri mteule wa CCM ambaye licha ya harakati ndani ya chama hicho bado hajafahamika.

Mwenyekiti wake Freeman Mbowe anapewa sifa ya kuweza kuwamudu nakuwavumilia makada wa chama hicho wengi wakiwa vijana wenye mihemko ya kisiasa na kutaka hatua za haraka katika mambo mengi.

Wachunguzi wa siasa ndani ya Chadema, wanasema uwezo wa Mbowe akiwa Mwenyekiti na Kiongozi wa Upinzani Bungeni ameweza kuwamudu wabunge vijana ambao ni machachari wakiwamo, Halima Mdee (Kawe), Ezekia Wenje (Nyamagana), Joseph Mbilinyi (Mbeya Mjini), Mchungaji Peter Msigwa (Iringa Mjini), Zitto Kabwe (Kigoma Kaskazini), Godbless Lema (Arusha Mjini) na wengineo.
Jaribu kubwa la Mbowe lilikuwa ni kauli za Mbunge wa Maswa Mashariki, John Shibuda ambaye mara kadhaa alitoa matamshi kinyume cha msimamo wa Chadema lakini Mbowe hakuwahi kukubali Chadema kupoteza muda katika suala hilo.

Hata hivyo changamoto katika chama hicho kikuu cha upinzani nchini ni jinsi kitakavyosimamia uchaguzi wake wa ndani mwaka 2014 na uteuzi wa mgombea wa urais na wabunge mwaka 2015.

Ndani ya CCM
Mwaka huu, ndani ya CCM jina la Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa lilitikisa vyombo vya habari hasa pale alipoamua kuvunja ukimya na kuweka bayana kile alichodai kuwa ni ukweli kuhusu sakata la Richmond ambalo limekuwa likimwandama tangu alipolazimika kuachia madaraka Februari 2008.

Lowassa katika NEC ya CCM iliyopita, aliweka wazi kwamba kumwandama kwa suala la Richmond ni kumwonea kwani hata Rais Jakaya Kikwete anafahamu kilichojiri.

Hata hivyo, wafuatiliaji wa siasa za ndani ya CCM wanaiona hatua hiyo ya Lowassa kwamba inamweka katika hatari kubwa ya kubanwa zaidi hasa kutokana na kumtaja Rais ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM kwamba alikuwa akijua kila kilichoendelea kuhusu Richmond.

Lowassa ni mmoja wa watu waliokuwa wakitajwa kwamba wanatakiwa kujivua gamba, mpango ulioasisiwa na Rais Kikwete kuwataka watuhumiwa wa kashfa mbalimbali hasa za ufisadi ndani ya chama hicho tawala, kuachia kwa hiari yao nafasi za uongozi walizonazo.

Tangu azimio la kuwataka watuhumiwa hao kujiuzulu kwa hiari yao litolewe ilipita miezi saba ambayo ilishuhudia historia ikiandikwa katika media ya siasa nchini, kufuatia kujiuzulu kwa Rostam.

Kujiuzulu kwa Rostam ambaye anatajwa kuwa mshirika wa karibu wa Rais Kikwete kwa upande mmoja na Lowassa kwa upande mwingine, ilitafsiriwa kuwa inadhoofisha moja ya makundi ambayo yamo ndani ya CCM.

Hata hivyo Rostam alijiuzulu huku akilalama kuhusu kile alichokiita siasa uchwara zinazoendeshwa ndani ya CCM na kuwataja, Nape Nnauye ambaye ni Katibu wa Itikadi na Uenezi wa chama hicho na Naibu Katibu Mkuu wa CCM (Tanzania Bara), John Chiligati kuwa chanzo cha siasa hizo.

Wanasiasa vijana
Nape ni mmoja wa wanasiasa vijana waliog’ara katika siasa za Tanzania 2011 hasa pale alipoteuliwa kuwa mmoja wa wajumbe wa Sekretarieti mpya ya CCM inayoongozwa na Katibu Mkuu, Willson Mukama.

Kung’ara kwa Nape kunatokana na kile kinachotajwa na wachunguzi wa siasa za hapa nchini kwamba ni ujasiri wa kusema bila woga kile anachokiamini, pasipo kujali wabaya wake ambao wamekuwa wakikwandama kwamba anasababisha mgawanyiko ndani ya chama chake.

Ujasiri wake huo ndio uliababisha kupangwa njama za kumvua wadhifa wake katika vikao vya juu vya CCM vilivyofanyika mwishoni mwa Novemba mwaka huu mjini Dodoma, mpango ambao hata hivyo haukupata hata nafasi ya kujadiliwa hasa pale suala la kujivua gamba liliporejeshwa Kamati Kuu kwa maana ya kuwashughulikia kinidhamu wale wote wenye makosa ambao hawakufuata nyayo za Rostam kujiuzulu nyadhifa zao.

Ndani ya vyama vya upinzani, David Kafulika ambaye ni Mbunge wa Kigoma Kusini kupitia NCCR Mageuzi alijikuta akitimuliwa uanachama pale alipoonekana kuwa tishio kwa mwenyekiti wake, James Mbatia.

Kafulila ambaye hata hivyo amri ya kufukuzwa kwake imesitishwa na Mahakama Kuu alikofungua kesi kupinga kufukuzwa huko, ni mwanasiasa ambaye amekuwa mahiri katika ujenzi wa hoja hasa ndani ya Bunge ambako aliwahi kuibua sokomoko pale alipowataja kwa majina wabunge watatu wa  CCM  kwa tuhuma za kupokea rushwa wakiwa kazini.

Suala hilo hadi leo limebaki kuwa kiporo kisichoguswa kwani Spika wa Bunge, Anne Makinda hajawahi kuthubutu  kutoa mwongozo ulioombwa na wabunge wawili kuhusu tuhuma hizo akiwamo Godfrey Zambi wa Mbozi Magharibi (CCM) ambaye ni mmoja mwa waliotajwa.

Mwanasiasa mwingine kijana ni January Makamba, mtoto wa Katibu Mkuu mstaafu wa CCM, Yusuph Makamba. January kama ilivyo kwa Nape ni mmoja wa wajumbe wa sekretarieti ya CCM inayoongozwa na Mukama.

Kadhalika Mbunge huyo wa Bumbuli ameiongoza Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini ambako yeye ni Mwenyekiti, kuibana Serikali hasa katika masuala ya umeme kiasi cha kutuhumiwa kwamba ana malengo binafsi ya kutaka kuwa Waziri wa Nishati na Madini, inayoongozwa na Waziri mwingine kijana, William Ngeleja.

Mbali na kuihenyesha Serikali katika masuala ya Umeme, kamati yake katika bunge lililopita iliibua uozo katika sekta ya gesi, pale ilipoweka bayana kwamba Kampuni ya Pan African Energy imekuwa ikiibia Serikali Tanzania mamilioni ya fedha.

Zitto Kabwe ambaye ni Naibu Katibu Mkuu wa Chadema na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, ameendelea kuwa kipenzi cha Watanzania wengi hasa vijana licha ya ujio wa vijana wapya hasa katika Bunge ambako aliibukia mwaka 2005.

Zitto katika siku za karibuni ameonyesha umahiri mkubwa katika masuala ya fedha na uchumi, amekuwa akivutana na Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustapha Mkulo kuhusu hali ya uchumi na nchi.

Wakati wa Bunge la Bajeti alivutana na Mkulo kiasi cha kuweka nadhiri kwamba ikibainika kwamba amekula rushwa angejiuzulu Ubunge, huku akimtaka Mkulo naye kuweka nadhiri hiyo. Mkulo hakukubali.

Tundu Lissu ambaye ni Mbunge wa Singida Mashariki akiwa mgeni katika siasa za Bunge, amekuwa mwiba mkali katika masuala ya utunzi wa sheria na mara kadhaa amekuwa akiwahenyesha wabunge wa CCM na Serikali bungeni.

Hotuba yake ya mwisho bungeni ni kuhusu muswada wa sheria ya marekebisho ya Katiba, ambayo ilifanya uchambuzi wa nafasi ya Tanzania Zanzibar katika muungano kiasi cha kuwakasirisha sana wabunge wa Visiwani humo.

Chadema waliamua kutoka nje kutokubaliana na kuendelea kujadiliwa kwa muswada huo ambao walisema kuingizwa kwake bungeni na kusomwa kwa mara ya pili, kulikuwa ni batili kwani ulitakiwa usomwe kwa mara ya kwanza kutokana na mabadiliko mengi ikiwa ni pamoja na kuandikwa kwa Kiswahili.

Ndani ya CUF
CUF wanahitimisha mwaka 2011 wakiwa katika mgogoro mkubwa wa kiongozi kufuatia vita baina ya Katibu Mkuu wake, Maalim Seif Sharif Hamad na Mbunge wa Wawi, Hamad Rashid Mohamed ambaye anataka kuwania nafasi ya Seif.

Mgogoro huo unaendelea kukiweka chama hicho katika wakati mgumu hasa ikizingatiwa kwamba kuingia kwake katika maridhiano na CCM na kuunda Serikali ya umoja wa kitaifa Tanzania Visiwani kulikiathiri kwa kiasi kikubwa.

Katika baadhi ya uamuzi wake hasa ndani ya Bunge, CUF kimekuwa kikionekana kuegemea upande wa Serikali na mara kadhaa kumekuwa na tuhuma kwamba ni CCM ‘B’.

Katika uchaguzi wa Igunga mgombea wake Leopold Mahona alipata kura zaidi ya 2,000 zikiwa ni pungufu kwa kura 7,000 ikilinganishwa na idadi ya kura ambazo mgombea huyo huyo alipata katika uchaguzi wa 2010.


Hizo ni baadhi ya takwimu zinazoonesha wazi jinsi ambavyo mwaka 2011 ulivyokua na upinzani na mikwarunzano ya hapa na pale hususani katika medani nzima ya siasa hapa nchini, Katika hayo viongozi wanapaswa kujifunza na kuepuka mikwaruzano inayoweza kuleta maafa kwa jamii hususani katika mwaka huu mpya wa 2012.                                                                                       

Monday, December 19, 2011

YALIYOJILI ZAIDI WAKATI WA BUNGE LA BAJETI 2011/2012.

Kamati ya Fedha na Mipango wakijadiliana dakika za mwisho kabla ya kuwasilisha Bajeti Bungeni

Wabunge la Bunge la TUSO-IUCo 2011/12 wakifuatilia kwa makini uwasilishaji wa Bajeti

Mh Mbunge akielekeza jambo fulani

Waziri wa Elimu

Waziri wa Makazi,Mh.Nativity.

"Kama hakuna watu sina sababu ya kupeleka ulinzi ukumbini" majibu ya Waziri wa Ulinzi na Usalama TUSO-IUCo 2011/12 kwa wabunge "

Mh Catherine Moshi,kaimu Waziri wa Habari na Mahusiano ya Umma akisoma bajeti ya Wizara mbele ya Bunge Tukufu la TUSO-IUCo.

"Burudani ndo kila kitu bwana",Waziri wa Michezo,Burudani na Utamaduni akisoma bajeti ya wizara yake.

"Mkinipa Milioni moja,nawahakikishia ifikapo January 2012 Website ya wizara itakuwa imeshaanza kufanya kazi,nipatieni hii hela jamani",maneno ya Waziri wa Mambo ya nje Mh.Ezekiel akitetea bajeti yake ipitishwe mapema jana.

Chakula kwa afya bora; Naibu Waziri wa Chakula na afya akiwasilisha.

Na hapa ndo nyumba ambapo maadili yote yanapatikana Bwana.Waziri wa maadili akiwasilisha.

Waziri wa Fedha na Mipango Wakipongezana na Spika wa Bunge baada ya Bunge la tano la 2011/12 kuahirishwa.

Spika wa Bunge akifafanua jambo wakati wa uwasilishaji wa bajeti

Waziri wa Fedha na Mipango zamu yake ilifika ya kuwasilisha bajeti Bungeni.


Zamu ya kuwasilisha bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu iliwadia,na hapa Waziri Mkuu,Mh Richardson akiwasilisha 



SERIKALI YA WANAFUNZI CHUO CHA TUMAINI,WAWASILISHA BAJETI ZA WIZARA ZAO BUNGENI.

Waziri wa Elimu kutoka Chuo cha Tumaini tawi la Mbeya akiwasilisha bajeti ya wanachuo wa Mbeya
Mbunge wa Tumaini mbeya
Waziri wa Sheria na Katiba akiomba mwongozo kwa Spika

Waziri wa Sheria na Katiba akiwasilisha Sheria ya wizara yake.

Thursday, December 8, 2011

Habari zaidi katika picha juu ya mvua zilizonyesha mkoani Iringa.

b
                        Mtoto huyu anatafuta samaki kwa njia ya mkono
            Na kweli akafanikiwa kupata samaki aina ya kambale kama inavyoonekana hapo juu

         Mvua ilipozidi kunyesha mambo yalikua hivi, maji ya kutosha kwenye nyumba za watu.
                                                                                                              
                                                                                                                                         Na Frank Kimaro

Wednesday, December 7, 2011




.
 Mojawapo ya nyumba zilizokumbwa na maji Tumaini.


Na John Alex


Mvua zinazoendelea kunyesha katika maeneo tofauti mkoani Iringa zimepelekea baadhi ya  njia kadhaa za  maeneo tofauti ya manispaa ya Iringa  kupitika kwa shida kutokana na  kufurika kwa mifereji na vijito vya maji hali inayosababisha  miundombinu  ya barabara na madaraja kupoteza ubora wake na  kuanza kuharibika.

Hali hii imrjitokeza katika maeneo kadhaa yamanispaa ya Iringa ambapo  baadhi ya maeneo hususan maeneo ya Semtema , Kihesa ,na  maeneo ya chuo kikuu cha Tumaini  njia zake  kufurika maji wakati wa mvua  hali inayopelekea wakazi wa maeneo hayo kupita kwa shida  kwenye madaraja ambayo wakati wa mvua yalifurika  maji.

Mvua zilizonyesha  siku ya jumaatano  zilifurisha  mifereji na  mito  katika maeneo hayo hali iliyosababisha usumbufu mkubwa sana kwa wakazi wa  maeneo hayo kupita kwa shida kwenye madaraja  ambayo yalijaa maji na kufanya  miundombinu  kuwa katika hatari ya kuharibika

Aidha mvua hizo zimehatarisha  baadhi ya nyumba zilizojengwa pembezoni mwa  mito na mifereji kwani  maji yalikaribia  karibu  na kuta za nyumba zilizoko kwenye maeneo ya  pembezoni mwa  mifereji hiyo.
Wakazi wa Semtema  wamesema kuwa mvua hizo  zilizonza kunyesh a hivi kariibuni  endapo zitaendelea kunyesha  zitaharibu miundombinu  ya barabara na madaraja kwani  hayakujengwa kwa  kiwango kinachotakiwa kuhimili mafuriko na mvua zilizokithiri.

Hata hivyo hali hiyo imejitokeza pia katika maeneo ya Zahanati  maeneo ya Mwangingo ambapo baadhi ya nyumba ziliingia maji na kusababisha wasiwasi mkubwa kwa wakazi wenye nyumba zao maeneo pembezoni mwa mto   kuhofia kukosa makazi  baada ya kushuhudia  maji yakiingia hadi ndani.

Wakazi wa maeneo hayo wamesema kuwa  endapo mvua hizo zitaendelea kunyesha zitaleta maafa makubwa ikiwa ni  pamoja na kupoteza maakazi  kwa  wananchi waliojenga nyumba zao pembezoni mwa  mito.

Hata hivyo baadhi  ya wakazi wa manispaa ya Iringa wameliambia kwanza jamii kuwa  mvua zinazoendelea kunnyesha zitapnguza ukame na  hivyo kufanya shughui za kilimo kuendelea vizuri lakini endapo zitaitiliza zinaweza ziksababisha hasara kwa mazao.

Mvua hizo zimesababisha uharibifu mkubwawa bostani za mbogamboga hususan kwa wakazi wa Tumaini ambao wamekuwa wakijihusisha na kilimo cha bostani za mbogamboga pembezoni mwa mto .